Na Mwandishi Wetu, Arusha
WADAU mbalimbali wa maendeleo katika sekta ya kilimo nchini wameridhishwa na utekelezaji wa mradi wa ‘Biodiversity for Opportunities, Livelihoods and Development’ (BOLD), unaolenga kuinua sekta ya mbegu kwenye nchi zaidi ya 50 duniani ikiwemo Tanzania, kupitia tafiti zinazoendelea kufanyika.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti pembezoni mwa warsha inayoendelea ya wadau wa mnyororo wa thamani wa rasilimali za vinasaba vya mimea inayofanyika kwenye Taasisi ya Kimataifa ya Utafiti na Uendelezaji wa Kilimo cha Mbogamboga Kanda ya Mashariki na Kusini mwa Afrika (World Vegetable Center) jijini hapa, wameelezea kufurahishwa na utekelezaji wa mradi huo.
Mratibu wa mradi huo kutoka Global Crop Diversity Trust (Crop Trust), Benjamin Kilian amesema mradi huo utakuwa mkombozi kwa wakulima wadogo, kwani umebeba malengo saba yatakayo leta matokeo endelevu kwenye tafiti za mbegu sambamba na kuongeza uzalishaji na uchakataji wa mazao yaliyosahaulika.
Aliongeza kuwa siku tano, watashiriki pia katika vikao vya ushirikiano, mijadala ya sera, na ziara za shambani ili suluhisho za pamoja zinazoweza kutekelezeka kwa mifumo ya chakula imara na jumuishi.
Aidha, Kilian aliipongeza Taasisi ya WorldVeg kwa kuwakutanisha pamoja wadau katika sekta ya kilimo, na kubainisha kuwa wamekuwa wakisaidia benki za kitaifa za vinasaba duniani kote, na Tanzania ni miongoni mwa washirika wao wakubwa.
Kwa upande wake Mkuu wa Kitengo cha Taifa cha Hifadhi ya Nasaba za Mimea kutoka Mamlaka ya Afya ya Mimea na Viuatilifu Tanzania (TPHPA), Dk. Mujuni Sospeter Kabululu amesema kwa upande wa Tanzania, wanashiriki katika vifurushi vitatu vya kazi kati ya vile saba, kwa kuangalia jinsi watakavyoimarisha mifumo ya mbegu, mifumo ya uhifadhi katika mazao manne ambayo ni ulezi, njugumawe, viazi vitamu na moringa.
“ Mazao haya yalichaguliwa kupitia kikao cha wadau tulichokaa kuchagua ni aina gani ya mazao yaingizwe kwa ajili ya kuyafanyia tafiti pamoja na kuongeza matumizi yake,” amesema Dk Kabululu.
Naye Mkurugenzi Mkaazi wa WorldVeg, Colleta Ndunguru amesema wamekuwa na wasaa mzuri kwani mradi huo umeweza kuwaweka pamoja wataalamu zaidi ya 40 kujadili namna bora ya kuhifadhi nasaba za mimea pamoja na kuhifadhi mbegu za asili sambambana kubadilishana uzoefu utakaochangia kukuza sekta ya mbegu duniani.
“Tumekuwa tukifanya kazi kwa karibu na wadau wetu ambao ni Mamlaka ya Afya ya Mimea na Viuatilifu Tanzania (TPHPA), Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI) pamoja na Taasisi ya Kuthibiti Ubora wa Mbegu Tanzania (TOSCI) katika kubadilishana uzoefu na ujuzi utakao tusaidia kuzalisha mbegu zinazohimili magonjwa pamoja na kukabiliana na mabadiliko ya tabia ya nchi,” alisema Ndunguru.
Naye Dk Adolf Saria kutoka TOSCI, amesema mradi huo utasaidia kuhakikisha mbegu ambazo zimesahaulika zinapata nafasi.




